TRENDING NOW






Njombe: Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe imetangaza kuendesha kambi maalum ya madaktari bingwa na bingwa bobezi kuanzia tarehe 23 hadi 27 Machi 2026 kwa lengo la kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi wa mkoa huo na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe chini ya Wizara ya Afya Tanzania, kambi hiyo itahusisha madaktari wabobezi katika fani mbalimbali za tiba ili kusaidia wananchi kupata uchunguzi, ushauri na matibabu ya magonjwa mbalimbali.

Huduma zitakazotolewa katika kambi hiyo ni pamoja na matibabu ya magonjwa ya ndani kama kisukari, magonjwa ya moyo, figo na shinikizo la damu. Aidha, wananchi watapata huduma za kibingwa za macho, sikio, pua na koo pamoja na huduma za upasuaji wa mifupa na upasuaji wa jumla.

Vilevile kutakuwa na huduma za kibingwa kwa watoto, wanawake na uzazi, pamoja na matibabu ya ubingwa bobezi yanayohusu mfumo wa chakula, magonjwa ya moyo na mfumo wa mkojo. Huduma nyingine zitakazopatikana ni pamoja na radiolojia, dawa za usingizi na ganzi salama pamoja na huduma za kinywa na meno.

Akitoa taarifa hiyo kwa umma, Afisa Uhusiano wa hospitali hiyo, Ombeni S. Utembele, amewahimiza wananchi wenye changamoto za kiafya kufika hospitalini hapo katika tarehe zilizotajwa ili kupata uchunguzi na matibabu stahiki.

Amesema huduma hizo zitatolewa kwa gharama za kawaida za hospitali na pia zitahusisha matumizi ya bima za afya, huku akisisitiza kuwa hospitali hiyo ipo tayari kuwahudumia wananchi wote kwa ubora.

Kambi hiyo inatarajiwa kuwasaidia wananchi wengi wa Mkoa wa Njombe kupata huduma za kibingwa bila kusafiri umbali mrefu kwenda katika hospitali nyingine kubwa nchini.

Na Mwandishi Wetu, Kilimanjaro

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa Shilingi Bilioni 25 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa Kikao cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Jeshi la Polisi kilichofanyika mwaka 2024 lengo ikiwa kuifanyia maboresho Shule cha Polisi Kilimanjaro ambacho kinakabiliwa na uchakavu wa Majengo ambayo yalijengwa tangu mwaka 1933 ambapo yanajumuisha Mabweni ya Wanafunzi, Madarasa na Nyumba za Askari.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama(NUU) iliyotembelea shule hiyo kukagua matumizi ya fedha hiyo iliyotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ikiwa ni utaratibu wa Kamati za Bunge kufuatilia matumizi ya fedha zinazotolewa na serikali kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Leo tunazungumza Wizara ya Mambo ya Ndani ambapo Rais ameweza kuyafanya haya ambayo wajumbe mmeyashuhudia leo kwa kiasi cha Shilingi Bilioni 25 ambazo mmeona kwa kiwango kikubwa na uweledi mkubwa wa jeshi katika utekelezaji na uwezo wa kusimamia kazi.Kwa kweli hatuna namna ya kuweza kumshukuru Mheshimiwa Rais Zaidi ya kumuombea afya njema,umri na rizki ili Mwenyenzi Mungu aendelee kumpa hekima na busara ili sisi wizara tuendelee kuwa wanufaika wa uongozi wake” amesema Waziri Katambi.

“Lakini tuna miradi ya ujenzi wa nyumba sehemu mbalimbali ambapo Mheshimiwa Rais pia anatoa kiasi kikubwa cha fedha na pale Dodoma tayari mradi ushaanza na tunatumia wataalamu wetu wa ndani na wanajenga kwa viwango vile vile kama mlivyoona hapa Shule ya Polisi,tunaenda kufanya maboresho ya maslahi kwa askari,mabadiliko ya sera na sheria na teknolojia za kisasa pia zinaendelea kuingizwa jeshini ili vifaa vya kisasa vitumike katika kulinda usalama wetu.” Aliongeza Waziri Katambi.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya NUU, Najma Murtaza Giga, ametoa pongezi kwa Jeshi la Polisi kwa kujenga mradi huo kwa ufanisi na uweledi mkubwa huku akikiri kuona thamani ya kiasi cha fedha kilichotolewa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan huku akiweka wazi Kamati kuendelea kuwa na imani na Jeshi la Polisi katika masuala mbalimbali na hivyo haina budi kuendelea kulisemea Jeshi la Polisi kuhakikisha linawezeshwa ili liweze kutekeleza majukumu yake ya kulinda usalama wa raia na mali zao kwa weledi na ufanisi wa hali ya juu.

Nae Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, ameishukuru Kamati hiyo ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) kwa kutenga muda na kuona umuhimu wa kutembelea Shule ya Polisi Tanzania-Moshi mkoani Kilimanjaro na kuona thamani ya fedha iliyotolewa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inavyotumika kwa kuhakikisha ubora na ufanisi unaonekana kwenye miradi hiyo ya ujenzi.

Aidha, IGP Wambura, ameiambia kamati hiyo kuwa, serikali ya awamu ya sita imeendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi kwenye miundombinu mbalimbali kote nchini ili kuhakikisha askari Polisi wanafanya kazi kwenye mazingira mazuri na wezeshi katika kuwahudumia wananchi, kutatua kero mbalimbali ili waendelee kufanya kazi zao bila uwepo wa matishio ya kihalifu nchini.

Na Mwandishi Wetu.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za dini nchini katika kulinda amani, kuimarisha maadili na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo Jumapili (Machi 15, 2026) wakati akitoa salamu katika Ibada iliyofanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Mpanda Mjini, Dayosisi ya Ziwa Tanganyika, iliyoongozwa na Askofu Imani Ahobokile Chibona.

Amesema Serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na taasisi za dini katika kujenga Taifa lenye hofu ya Mungu, upendo, haki na uwajibikaji.

“Nimekuja pia na salamu za upendo kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye anatambua mchango mkubwa wa taasisi za dini katika kudumisha amani, maadili mema na mshikamano wa kitaifa,” amesema.





Waziri Mkuu amesema taasisi za dini zimekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi, hususan katika sekta za elimu, afya na malezi ya jamii.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuwekeza katika miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Katavi ikiwemo miradi ya maji, barabara na nishati kwa lengo la kuboresha huduma kwa wananchi.

Akizungumzia sekta ya maji, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea kutekeleza Mradi wa Maji wa Miji 28 ambapo jana aliweka jiwe la msingi la mradi wa kusambaza maji kutoka Bwawa la Milala unaotarajiwa kuzalisha lita milioni 12 za maji kwa siku na kuhudumia wakazi wa Manispaa ya Mpanda.

Katika sekta ya miundombinu, amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa barabara ya Mpanda – Tabora yenye urefu wa kilometa 352 kwa kiwango cha lami ambayo imekuwa kichocheo cha maendeleo ya kiuchumi katika mkoa huo.

Aidha, amesema ujenzi wa barabara ya Mpanda – Uvinza – Kanyani unaendelea ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 15.7, huku ujenzi wa barabara ya Kagwira – Karema nao ukiendelea kwa lengo la kufungua fursa za kiuchumi katika ukanda wa Ziwa Tanganyika.

Waziri Mkuu pia amesema Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa nishati ya umeme katika Mkoa wa Katavi ambapo vijiji vyote 172 tayari vimeunganishwa na umeme huku vitongoji 534 kati ya 912 vikifikishiwa huduma hiyo.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amewataka Watanzania kuendelea kulinda amani, umoja na mshikamano wa kitaifa akisisitiza kuwa amani ya nchi ni matokeo ya jitihada za pamoja za Serikali, taasisi za dini na wananchi.

“Taifa letu limeendelea kuwa kisiwa cha amani kwa sababu ya mshikamano wa Watanzania. Tuendelee kuwa mabalozi wa amani katika familia, maeneo ya kazi na katika jamii kwa ujumla,” amesema.

Akizungumzia umuhimu wa kudumisha amani, umoja na mshikamano, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema kuwa mnufaika namba moja wa amani ni mwananchi mwenyewe na Taifa kwa ujumla.

“Tunapaswa kuepuka migogoro isiyo ya lazima hususan ya ardhi. Hata tukigombana au kupigana ardhi haiongezeki. Kilicho muhimu ni kukaa pamoja, kuzungumza na kushirikishana ili kutumia ardhi yetu kwa manufaa ya wote,” amesema.

Amesema kuendelea kwa migogoro ya ardhi kunaweza kuliweka Taifa katika mazingira yasiyo mazuri na kupelekea chuki pamoja na kuvunjika kwa umoja wa kitaifa. Ameongeza kuwa msingi wa maendeleo ya Taifa lolote ni amani, umoja na mshikamano, hivyo ni muhimu kuendelea kuliombea Taifa lisipoteze tunu hizo.

Kwa upande wake, Askofu wa Dayosisi ya Ziwa Tanganyika, Dkt. Imani Ahobokile Chibona, amesema Kanisa linaendelea kuhimiza waumini kudumisha amani, mshikamano na maadili mema katika jamii kwani amani ya Taifa inaanza na mtu mmoja mmoja katika familia na jamii.

Askofu Chibona pia ameitaka jamii kuendelea kuwaombea viongozi wa kitaifa ili Mungu awape hekima, nguvu na afya njema katika kuliongoza Taifa, huku akisisitiza kuwa Serikali imeendelea kufanya kazi kubwa ya kuwaletea wananchi maendeleo katika sekta mbalimbali.

Na Mwandishi Wetu.

Matukio yaliyoripotiwa katika kijiji cha Singisi ndani ya Wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha, yanaibua maswali mengi kuhusu mwenendo wa maadili na uwajibikaji wa baadhi ya vijana katika jamii ya sasa. Kwa mujibu wa taarifa zilizosambaa kupitia mitandao ya kijamii, kumekuwa na mfululizo wa vifo vya vijana katika mazingira yanayozua taharuki kubwa kwa wananchi wa eneo hilo.

Chanzo cha hofu hiyo kinadaiwa kuhusishwa na tukio lililotokea tarehe 29 Oktoba 2025, ambapo baadhi ya vijana walihusishwa na kitendo cha kuvamia na kuiba mali katika sheli ya Panone. Baada ya tukio hilo, mmiliki wa sheli hiyo alidaiwa kutoa tamko kali akisisitiza kuwa mtu yeyote aliyegusa mali katika tukio hilo anatakiwa kurejesha au kulipia, huku namba za mawasiliano zikiachwa ili wahusika waweze kuwasiliana. Tamko hilo limeendelea kuzungumzwa sana na wananchi, na baadhi yao wakihusisha matukio ya vifo vinavyoendelea na tukio hilo la awali.

Hata hivyo, zaidi ya hoja za kiimani au imani za wananchi, tukio hili linafungua mjadala mpana kuhusu mwenendo wa baadhi ya vijana wa kizazi cha sasa katika kuheshimu mali za watu wengine. Kumekuwa na tabia inayokua ya baadhi ya vijana kuamini kuwa wanaweza kupata mali kwa njia za mkato bila kufikiria madhara yake ya kisheria, kijamii au hata kiimani.

Kimsingi, jamii yoyote haiwezi kusimama bila misingi ya kuheshimu haki na mali za wengine. Wizi au uharibifu wa mali za watu sio tu unamdhuru mhanga wa tukio, bali pia unaathiri taswira ya vijana wote katika jamii. Matokeo yake ni kupotea kwa uaminifu, kuongezeka kwa hofu, na wakati mwingine kuzuka kwa simulizi na imani zinazoongeza taharuki miongoni mwa wananchi kama inavyoonekana katika tukio hili la Singisi.

Ni muhimu vijana kutambua kuwa mafanikio ya kweli yanapatikana kupitia juhudi, nidhamu na kuheshimu sheria na mali za wengine. Badala ya kuchukua mali kwa njia zisizo halali, vijana wanapaswa kujenga utamaduni wa kufanya kazi, kulinda mali za jamii, na kuwa mfano bora kwa vizazi vinavyokuja.

Aidha, jamii, viongozi wa mitaa, pamoja na wazazi wana jukumu kubwa la kuendelea kuwalea vijana katika maadili mema, kuwahimiza kuwajibika na kuwafundisha thamani ya uadilifu. Bila kufanya hivyo, matukio kama haya yataendelea kujirudia na kuacha majeraha makubwa katika jamii.

Kwa ujumla, tukio la Singisi linapaswa kuwa funzo kwa vijana wengi: kuheshimu mali za watu siyo tu suala la sheria, bali ni msingi wa utu, maadili na amani ya jamii.

Vatican City. Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Leo XIV, amemteua mchumi wa maendeleo kutoka Cameroon, Dk. Vera Songwe, kuwa mwanachama wa Pontifical Academy of Social Sciences, taasisi ya Vatican inayolishauri Kanisa Katoliki kuhusu masuala ya kijamii, kiuchumi na kisiasa duniani.

Kupitia uteuzi huo, Dk. Songwe anaungana na kundi la wasomi mashuhuri kutoka mataifa mbalimbali wanaofanya tafiti na kutoa ushauri kwa Kanisa kuhusu changamoto za maendeleo ya dunia, haki za kijamii na ustawi wa jamii.

Kabla ya uteuzi huo, Dk. Songwe aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali katika mfumo wa United Nations, ikiwemo kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja huo na Katibu Mtendaji wa United Nations Economic Commission for Africa. Katika nafasi hizo, alihusika katika kuandaa sera na mikakati ya kuimarisha maendeleo ya uchumi barani Afrika.

Taasisi ya Pontifical Academy of Social Sciences ilianzishwa mwaka 1994 kwa lengo la kukusanya wataalamu wa kimataifa kutoka fani mbalimbali kama uchumi, sosholojia, sheria na sayansi ya siasa ili kusaidia Kanisa Katoliki kuelewa na kutoa mwongozo kuhusu changamoto za kijamii na kiuchumi zinazoikabili dunia.

Ingawa wanawake hawaruhusiwi kuwa mapadre au maaskofu ndani ya Kanisa Katoliki, katika miaka ya karibuni Vatican imeanza kuwateua wanawake wachache katika nafasi za juu za ushauri na uongozi.

Kwa mujibu wa wachambuzi wa masuala ya Kanisa, uteuzi wa Dk. Songwe ni hatua muhimu katika kuongeza ushiriki wa wanawake katika taasisi za juu za Kanisa Katoliki duniani. Kutoka barani Afrika, anatajwa kuwa mwanamke wa tatu kuwahi kuteuliwa katika nafasi hiyo na Papa.

Hatua hiyo pia inaonekana kuimarisha mchango wa wasomi wa Afrika katika majadiliano ya kimataifa kuhusu maendeleo ya kijamii na kiuchumi duniani.

Dar es Salaam. Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dar es Salaam imetupilia mbali shauri la mapitio lililofunguliwa kupinga uundwaji wa Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba 2025.

Shauri hilo la Mapitio Namba 32537 la mwaka 2025 lilifunguliwa na Rosemary Mwakitwange pamoja na wenzake watatu dhidi ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wajumbe wa Tume hiyo ya Uchunguzi.

Katika maombi yao, walalamikaji waliiomba Mahakama Kuu ya Tanzania itoe amri ya kufuta uamuzi wa Samia Suluhu Hassan wa kuunda na kuteua wajumbe wa Tume hiyo tarehe 18 Novemba 2025, wakidai kuwa Rais alivuka mipaka ya mamlaka yake ya kisheria wakati wa kuunda chombo hicho.

Hata hivyo, baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Mahakama Kuu tarehe 13 Machi 2026 ilitupilia mbali shauri hilo, ikieleza kuwa Rais alitumia mamlaka yake kwa mujibu wa sheria wakati wa kuunda Tume hiyo.

Katika uamuzi wake, Mahakama ilieleza kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Tume za Uchunguzi, kifungu cha 3 kinampa Rais mamlaka ya kuunda Tume ya Uchunguzi na kuteua wajumbe wake.

Mahakama ilibainisha pia kuwa hakuna ushahidi uliowasilishwa unaoonesha kuwa Rais alivunja sheria au kwenda kinyume na matakwa ya sheria hiyo wakati wa kuunda Tume hiyo.

Aidha, Mahakama haikuona dalili ya upendeleo katika uteuzi wa wajumbe wa Tume, ikisisitiza kuwa sheria inampa Rais mamlaka ya kufanya uteuzi huo bila kuwekewa masharti ya ziada.

Kutokana na hoja hizo, Mahakama ilihitimisha kuwa maombi ya walalamikaji hayakuwa na msingi wa kisheria, hivyo ikaamua kuyatupilia mbali.

Shauri hilo liliendeshwa na jopo la mawakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, waliowakilisha Serikali katika shauri hilo.

Uamuzi huo unathibitisha uhalali wa kisheria wa uamuzi wa Rais wa kuunda Tume ya Uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani yaliyoripotiwa kutokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 nchini.


Na Mwandishi Wetu

Wananchi na wakazi wa Hydom wilayani Mbulu mkoa wa Manyara wamemshukuru Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia Wizara ya Maji kupitia RUWASA kutekeleza mradi mkubwa wa Majisafi ya bomba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41 na tayari vijiji vinne vimeshaanza kunufaika na mradi huo.

Wametoa pongezi hizo wakati wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira alipotembelea na kukagua mradi huo ikiongozwa na Mwemyekiti wake Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) katika eneo la Hydom lilipo tangi kubwa la ujazo wa lita 2,000,000 la mradi huo.

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA Mha. Wolta Kirita aliieleza Kamati hiyo kuwa tayari wananchi zaidi 800 wameshasajiliwa na kupatiwa kadi za malipo kabla ya matumizi kwani mradi huo unaenda sambamba na ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla, ambapo mwananchi anaweza kuchota maji kwenye kituo muda wowote anapokuwa anahitaji huduma hiyo.

Mkurugenzi Mkuu Kirita alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika Novemba 2027.

Kwa mujibu wa Meneja wa RUWASA mkoa wa Manyara Mha. James Kionaumela alisema mradi huo umeshaanza kutoa huduma katika vijiji vinne na ukikamilika utahudumia zaidi ya wakazi 100,000 wa eneo hilo.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga alisema kwa sasa wananchi wa wilaya hiyo wanapata maji kwa saa 12 kwa siku huku akiipongeza RUWASA kwa kazi nzuri katika kutekeleza mradi huo.











Ofisi ya BAKWATA Mkoa wa Singida, kupitia Sheikh wa Mkoa huo Issa Bin Nassoro, imezipongeza taasisi za Ramadhan Charity Programme2026, inayoongozwa na Ndugu Ahmed Misanga pamoja na Taasisi ya JAI Tanzania kwa kutoa sadaka katika Gereza la Manispaa ya Singida, misikiti pamoja na vituo vya watoto yatima.


Sheikh Issa amesema hayo leo wakati wa ziara yake ya kutembelea wafungwa katika Gereza la Manispaa ya Singida, ambapo pia walitoa sadaka ya Iftar kwa wafungwa ili waweze kupata futari pamoja na daku katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani. Sadaka hizo zimetolewa na taasisi za Ramadhan Charity Programme 2026 pamoja na JAI Tanzania.

Katika hotuba yake, Sheikh Issa aliwaomba watu mbalimbali katika jamii kuwajali watu wenye mahitaji na masikini, akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni jambo linalompendeza Mungu. Aliongeza kuwa hata mitume waliwahudumia na kuwasaidia watu masikini na wenye uhitaji.

Aidha, Sheikh wa Mkoa alitoa salamu kutoka kwa Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dkt. Abubakar Zubeir bin Ally, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwajali watu wenye mahitaji maalum, wakiwemo wafungwa na makundi mengine yenye uhitaji katika jamii.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Ramadhan Charity Programme 2026, Ndugu Ahmed Misanga, amesema kuwa utoaji wa sadaka ya Iftar kwa watu wenye mahitaji ni utaratibu wao wa kila mwaka, hususan katika magereza na makundi mengine ya jamii. Amesema kuwa wamekuwa wakifanya shughuli hiyo kwa zaidi ya miaka mitano sasa.

Misanga alisisitiza kuwa watu waliopo magerezani wanahitaji huruma na faraja kutoka kwa jamii ili kuwapa moyo na kuwasaidia kumkaribia Mungu, ili wanaporudi uraiani wawe watu wema wenye hofu ya Mungu na mchango chanya kwa jamii.

Katika msaada huo, Ramadhan Charity Programme 2026 kwa kushirikiana na JAI Tanzania walitoa sadaka ya Iftar iliyojumuisha boksi la tende, sukari, tambi, mchele, ngano, juisi pamoja na taulo za kike kwa ajili ya wafungwa wanawake katika gereza hilo.

Naye Kaimu Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Singida, Ndugu Amini Mjenza, amesema amefurahishwa na taasisi ya Ramadhan Charity chini ya uongozi wa Ahmed Misanga kwa kuwapatia sadaka ya Iftar, akieleza kuwa msaada huo utawasaidia sana wafungwa waliopo gerezani.

“Tutaitumia sadaka hii ya Iftar kama mlivyokusudia, na tunamuomba Mungu awalipie pale mlipotoa kwa ajili ya wafungwa wote, wanawake na wanaume,” amesema.
Katika tukio hilo, washiriki pia walipata nafasi ya kuliombea Taifa pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Taasisi ya Ramadhan Charity Programme 2026 imewataka Watanzania kutumia mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kuwa wamoja, kusaidiana na kufanya kazi kwa pamoja katika kuwasaidia wenye mahitaji katika jamii.