TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Dar es Salaam imeandika historia mpya katika harakati za kuboresha huduma za afya baada ya Mkoa wa Manyara kufanikisha zoezi kubwa la kuchangisha fedha lililowezesha kupatikana kwa zaidi ya Shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa njiti na kuimarisha huduma za afya katika mkoa huo.

Fedha hizo zilikusanywa kupitia hafla maalumu ya chakula cha jioni cha hisani (Manyara Tanzanite Marathon Dinner Gala) iliyofanyika Julai 24, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto, ambayo inalenga kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa, kuboresha huduma za watoto wachanga na kupunguza vifo vinavyotokana na kuzaliwa njiti.

Jumla ya Shilingi 1,356,900,000 zilipatikana kupitia ahadi za michango na fedha taslimu kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo, taasisi za fedha, makampuni binafsi, viongozi wa Serikali, wabunge, wafanyabiashara na wananchi waliojitokeza kuunga mkono kampeni hiyo.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa kitaifa na kikanda pamoja na wadau wa sekta ya afya, ambapo mshikamano mkubwa ulionekana katika jitihada za kuhakikisha watoto wanaozaliwa njiti wanapata huduma bora na salama.

Akizungumza baada ya harambee hiyo, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Babati Vijijini, Mhe. Daniel Baran Sillo, aliyekuwa mgeni rasmi, alisema mafanikio hayo yanaonesha moyo wa uzalendo na mshikamano wa Watanzania katika kusaidia sekta ya afya.

Alisema lengo la kampeni hiyo ni kufikisha zaidi ya Shilingi bilioni 1.5, huku akiwakaribisha Watanzania kushiriki Manyara Tanzanite Marathon itakayofanyika Agosti 22, 2026 mkoani Manyara.

“Tunawashukuru wadau wote waliojitokeza na kuchangia. Kila mchango una maana kubwa katika kuokoa maisha ya watoto wetu. Tunataka kuhakikisha hospitali zetu zinakuwa na vifaa vinavyohitajika kuwahudumia watoto njiti kwa kiwango cha kisasa,” alisema Mhe. Sillo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, alisema kampeni hiyo imeibuka kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha nguvu za Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto.

Aliwataka wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuchangia ili kufanikisha lengo lililowekwa, akisisitiza kuwa uwekezaji katika afya ya watoto ni uwekezaji katika mustakabali wa taifa.


“Kila mtoto ana haki ya kuishi. Tunapowekeza katika vifaa tiba na huduma za watoto njiti, tunaokoa familia, tunaimarisha jamii na tunajenga taifa lenye nguvu,” alisema Mhe. Sendiga.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, alieleza kuwa mkoa huo unakabiliwa na changamoto kubwa ya watoto wanaozaliwa njiti, ambapo kati ya watoto 3,000 hadi 3,200 huzaliwa njiti kila mwaka.

Alisema idadi hiyo inaweka shinikizo kubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya, hasa katika upatikanaji wa mashine za kusaidia watoto kupumua, incubators, vifaa vya ufuatiliaji wa afya za watoto wachanga na miundombinu ya huduma maalumu.
“Watoto njiti wanahitaji uangalizi wa karibu na vifaa maalumu. Bila uwekezaji wa kutosha, tunakuwa katika hatari ya kupoteza maisha ambayo yangeweza kuokolewa,” alisema Dkt. Method.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, kuzaliwa njiti ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia vifo vya watoto wachanga duniani, na huduma bora katika saa na siku za mwanzo baada ya kuzaliwa ndiyo huamua kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mtoto kuendelea kuishi.

Wadau waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa kampeni hiyo imeonesha mfano wa namna matukio ya michezo yanaweza kutumika kama nyenzo ya kuchangisha fedha kwa ajili ya miradi ya kijamii na maendeleo.
Mbio za Manyara Tanzanite Marathon zimekuwa zikikua kwa kasi na sasa zinatajwa kuwa moja ya matukio makubwa ya michezo na hisani nchini Tanzania, yakilenga kuhamasisha afya, utalii na maendeleo ya jamii kwa wakati mmoja.

Waandaaji wa marathon hiyo walisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika ununuzi wa vifaa tiba, uboreshaji wa huduma za watoto wachanga na kuimarisha uwezo wa hospitali za Mkoa wa Manyara kuhudumia watoto njiti kwa ufanisi zaidi.

Kampeni hiyo pia inaunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambazo zimekuwa zikilenga kuboresha huduma za afya, kupunguza vifo vya mama na mtoto, kuimarisha ustawi wa jamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika maeneo yote ya nchi.
Waandaaji wameendelea kutoa wito kwa Watanzania kushiriki mbio hizo au kuchangia kupitia akaunti maalumu za kampeni, wakisisitiza kuwa kila mchango ni hatua muhimu katika kuokoa maisha ya mtoto mmoja au zaidi.

Michango inaendelea kupokelewa kupitia CRDB Lipa Namba 113069180 na CRDB Account No. 10401215064 (Manyara Tanzania Marathon).

Kwa mafanikio yaliyopatikana katika usiku huo wa kihistoria, Mkoa wa Manyara umeonesha kuwa mshikamano wa jamii unaweza kuwa nguvu kubwa ya kuokoa maisha, huku kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto ikiendelea kuwa mwanga wa matumaini kwa maelfu ya watoto wanaozaliwa njiti kila mwaka nchini Tanzania.

Na Oscar Assenga, TANGA

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amewataka wananchi kuacha ukataji holela wa mikoko na kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wake, akisema misitu hiyo ni muhimu kwa kulinda fukwe, kuhifadhi viumbe wa majini na kuimarisha uchumi wa jamii za pwani.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, ameitaka jamii kuachana na tabia ya ukataji holela wa miti ya mikoko katika maeneo ya mwambao wa Bahari ya Hindi, akionya kuwa endapo vitendo hivyo vitaendelea vinaweza kuhatarisha makazi ya viumbe wa majini, maisha ya wananchi wanaotegemea rasilimali za bahari pamoja na usalama wa fukwe.

Dkt. Burian alitoa kauli hiyo Juni 28 wakati wa Maadhimisho ya Kitaifa ya Siku ya Uhifadhi wa Ikolojia ya Mikoko yaliyofanyika katika eneo la Donge Mnyanjani, Jijini Tanga.

Alisema Mkoa wa Tanga umebarikiwa kuwa na ukanda mpana wa pwani pamoja na misitu ya mikoko yenye umuhimu mkubwa wa kiikolojia na kiuchumi katika wilaya za Mkinga, Pangani, Muheza na Jiji la Tanga.

Alieleza kuwa mikoko ni ngao muhimu inayolinda mwambao wa bahari dhidi ya mmomonyoko wa ardhi, huku pia ikiwa mazalia ya samaki na makazi ya viumbe wengine wa majini wanaochangia kuimarisha sekta ya uvuvi na kipato cha wananchi wa maeneo ya pwani.

"Mikoko ya Tanga si tu inalinda mwambao wa bahari dhidi ya mmomonyoko wa ardhi, bali ni chanzo muhimu cha maisha ya wavuvi na jamii nyingi za pwani. Kwa miaka ya hivi karibuni Mkoa wa Tanga umeendelea kuwa mfano wa uhifadhi wa mazingira unaokwenda sambamba na maendeleo ya utalii wa ikolojia," alisema Dkt. Batilda Burian.

Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza umuhimu wa kurejesha maeneo yaliyoharibiwa kwa kupanda mikoko mipya ili kurejesha mazingira katika hali yake ya awali kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha, aliwataka viongozi wa serikali za mitaa, vikundi vya wavuvi, wanawake, vijana, wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo Scouts kuendelea kushiriki kikamilifu katika juhudi za uhifadhi wa mikoko huku wakizingatia sheria na taratibu za usimamizi wa misitu.

"Tunapanda mikoko leo, lakini bado tunakabiliwa na changamoto kubwa ya uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na mifuko ya plastiki, chupa na taka nyingine zinazotupwa ovyo kwenye fukwe zetu. Ni wajibu wetu kuendelea kutoa elimu kwa watoto na vijana kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mikoko, kwa sababu tunapohifadhi mikoko tunalinda maisha yetu, chakula chetu, uchumi wetu na mazingira ya watoto wetu," alisisitiza Dkt. Burian.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Kamishna wa Uhifadhi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Husein Msuya, alisema Siku ya Kimataifa ya Uhifadhi wa Ikolojia ya Mikoko huadhimishwa kila mwaka ifikapo Juni 28, baada ya kuanzishwa na UNESCO mwaka 2015 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa mifumo ya ikolojia ya mikoko na wajibu wa kuihifadhi.
Alisema Tanzania ina takribani hekta 158,100 za misitu ya mikoko iliyopo katika wilaya mbalimbali za ukanda wa pwani, zikiwemo Tanga, Pangani na Mkinga, ambapo misitu hiyo ina mchango mkubwa katika kuhifadhi bioanuwai, kuzuia mmomonyoko wa fukwe, kuhifadhi kaboni na kukuza uchumi kupitia uvuvi pamoja na utalii wa ikolojia.
Wananchi wahamasisha uhifadhi wa mikoko
Mkazi wa Jiji la Tanga, Abdalah Mwalimu, alisema wananchi wana wajibu wa kutunza mikoko kwa kuwa ndiyo kinga ya kwanza dhidi ya athari za mawimbi makubwa na mabadiliko ya tabianchi yanayoathiri maeneo ya pwani.

"Mikoko ni uhai wetu. Tukiiharibu, tutakuwa tumeharibu mazalia ya samaki, tumepunguza kipato cha wavuvi na kuhatarisha usalama wa fukwe. Kila mmoja wetu anapaswa kushiriki kupanda na kuitunza," alisema Abdalah Mwalimu.

Kwa upande wake, mkazi mwingine wa Jiji la Tanga, Fatuma Omari, alisema elimu ya uhifadhi wa mazingira inapaswa kuendelea kutolewa kwa wananchi wote ili kuongeza uelewa wa umuhimu wa kupanda mikoko na kulinda fukwe.

"Kupanda mikoko ni uwekezaji wa maisha ya baadaye. Tunapaswa kuwafundisha watoto wetu kupenda mazingira ili waendeleze jukumu hili na kuhakikisha fukwe zetu zinabaki salama kwa vizazi vijavyo," alisema Fatuma Omari.

Fatuma aliongeza kuwa ushirikiano kati ya wananchi, serikali na taasisi zinazoshughulika na uhifadhi wa mazingira ni muhimu katika kuhakikisha mikoko inaendelea kulindwa na kurejeshwa katika maeneo yaliyoharibiwa.

Abdalah naye alihimiza vijana kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kampeni za upandaji wa mikoko na usafi wa fukwe, akisema hatua hiyo itasaidia kuhifadhi mazingira, kuongeza uzalishaji wa samaki na kukuza uchumi wa jamii za pwani kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Salaam Maalum kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Mhe Xi Jinping iliyokabidhiwa kwake na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania ni Mhe. Chen Mingjian, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar tarehe 28 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania ni Mhe. Chen Mingjian, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar tarehe 28 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania ni Mhe. Chen Mingjian mara baada ya kumaliza mazungumzo yaliyofanyika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar tarehe 28 Julai, 2026.

Na Mwandishi Wetu, Arusha. 

Benki ya NMB imekabidhi udhamini wa Sh10 milioni kwa mwanariadha wa Tanzania, Alphonce Simbu, ili kumsaidia katika maandalizi ya kushiriki mbio za TCS Sydney Marathon 2026 zitakazofanyika Agosti 30, 2026 jijini Sydney, Australia.

Udhamini huo unalenga kumpunguzia Simbu changamoto za kifedha wakati wa maandalizi, ili aweze kuelekeza nguvu zake zote kwenye mazoezi na kuiwakilisha Tanzania vyema katika mashindano hayo ya kimataifa.

Akimkabidhi Simbu hundi ya udhamini huo jijini Arusha, Meneja wa NMB Kanda ya Kaskazini, Baraka Ladislaus, alisema benki hiyo imeamua kuwa sehemu ya safari ya mwanariadha huyo kutokana na rekodi yake ya kuendelea kuipeperusha bendera ya Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kimataifa.

Alisema NMB inaamini mchango huo utampa utulivu wa kufanya maandalizi yake bila vikwazo vya kifedha.

"Tunamwamini Simbu kwa sababu ameendelea kuiandikia Tanzania historia katika mchezo wa riadha. Tunaamini hata safari hii atafanya makubwa na kuendelea kulitangaza taifa letu," alisema Ladislaus.

Alimtakia Simbu maandalizi mema na mafanikio makubwa katika mashindano hayo.

Mbali na fedha hizo, NMB pia ilimkabidhi Simbu kadi ya benki pamoja na NMB Band, bangili ya malipo ya kidijitali inayotolewa kwa ushirikiano na Mastercard, ambayo itamwezesha kufanya malipo salama na kwa urahisi katika maeneo mbalimbali duniani yanayokubali Mastercard au Visa.

Kwa mujibu wa Ladislaus, huduma hiyo itarahisisha miamala ya kifedha ya mwanariadha huyo wakati wote wa safari na kipindi cha mashindano.

Akizungumza baada ya kupokea udhamini huo, Simbu alisema maandalizi yake yanaendelea vizuri na afya yake ipo katika hali nzuri huku akieleza kuwa analenga kutwaa medali ya dhahabu nchini Australia.

"Maandalizi yanaendelea vizuri na nina afya njema. Niko tayari kwa changamoto ya Sydney Marathon na nina imani kubwa ya kufanya vizuri. Lengo langu ni kurudi nyumbani na medali ya dhahabu," alisema Simbu.

Aliwataka Watanzania kuendelea kumuombea ili afanikiwe kutimiza ndoto hiyo na kuiletea nchi heshima.

Katika hatua nyingine, Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Rogath Steven, alisema maandalizi ya wanariadha yanaendelea vizuri chini ya usimamizi wa shirikisho.

Alisema Simbu pamoja na mwanariadha Magdalena Shauri wamekuwa wakifanya mazoezi katika eneo la Ilboru, Arusha, kutokana na mazingira na hali ya hewa inayofanana kwa kiasi kikubwa na ile ya Sydney.

"Maandalizi yanaendelea vizuri na tuna imani kubwa na wanariadha wetu. Tunaamini Tanzania ina nafasi nzuri ya kupigania medali ya dhahabu katika mashindano hayo," alisema Steven.

TCS Sydney Marathon ni miongoni mwa marathon kubwa duniani na mwaka huu inatarajiwa kushirikisha zaidi ya wakimbiaji 40,000 kutoka mataifa mbalimbali. Mbio za kilomita 42 zitaanzia Miller Street na kumalizikia katika eneo la Sydney Opera House Forecourt.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla (katikati), akimwakilisha Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, akikata utepe kuzindua rasmi Kituo cha Malezi ya Watoto cha Dkt. Hussein Ali Mwinyi kilichopo Mwanakwerekwe, Zanzibar. Wanaoshuhudia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Anna Athanas Maalim, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais  Ikulu, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Saada Mkuya Salum, na Afisa Mkuu wa Fedha wa Stanbic Bank Tanzania, Derick Lugemala. Kituo hicho kimefadhiliwa  na Benki ya Stanbic kinacholenga kupanua upatikanaji wa huduma bora za malezi, makuzi na elimu ya awali kwa watoto nchini Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, amefungua rasmi Kituo cha Malezi na Makuzi ya Awali ya Mtoto (ECD) cha Mwanakwerekwe kilichofadhiliwa na Stanbic Bank Tanzania, sambamba na uzinduzi wa Mpango wa Zanzibar wa Malezi na Makuzi ya Awali ya Mtoto wa Kisekta (2026–2031).

Ufadhili wa kituo hicho umetokana na awamu ya kwanza ya TZS milioni 350 iliyotolewa na Stanbic Bank Tanzania, ikiwa ni sehemu ya ahadi ya benki hiyo ya TZS milioni 500 kwa mpango wa Serikali wa Adopt an ECD unaoendeshwa na Shirika la Save the Children.

Kituo hicho kitatoa huduma bora za malezi na elimu ya awali kwa watoto wa wafanyabiashara na familia zinazofanya kazi katika Soko la Mwanakwerekwe na maeneo jirani.

“Uwekezaji huu unaakisi dhamira ya Stanbic Bank Tanzania ya kuendeleza malezi na makuzi ya awali ya mtoto kama msingi wa kujenga rasilimali watu, kukuza uchumi shirikishi na kuimarisha ustawi wa muda mrefu wa Zanzibar. Aidha, unaonesha mafanikio yanayowezekana pale Serikali, sekta binafsi na washirika wa maendeleo wanapounganisha nguvu kuelekea dira moja,” amesema Derick Lugemala, Afisa Mkuu wa Fedha, Stanbic Bank.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kituo hicho, Mhe. Hemed aliipongeza Stanbic Bank kwa kuunga mkono ajenda ya serikali ya kuwekeza katika maendeleo ya mtoto katika umri wa awali na kuzitaka benki nyingine pamoja na taasisi za kifedha kuiga mfano huo wa kuchangia maendeleo ya taifa.
 
"Tunaipongeza Benki ya Stanbic kwa uwekezaji huu wa kimkakati na mchango wake endelevu katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi, si Zanzibar pekee bali Tanzania nzima kwa ujumla. Nazihimiza benki nyingine na taasisi za kifedha kuiga mfano huu mzuri wa kushiriki katika ujenzi wa taifa," alisema kabla ya kukifungua rasmi kituo hicho kilichopewa jina la Kituo cha Malezi ya Watoto cha Dkt. Hussein Ali Mwinyi.